Tuesday, March 20, 2012

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MALIASILI NA UTALII

TAARIFA KWA UMMA

MABADILIKO KATIKA SEKTA YA MISITU

Ujumbe huu Ulitolewa kwa mara ya kwanza na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe Ezekiel Maige  kwa Wavunaji wakubwa wa misitu, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) na wadau wengine wa misitu
Sao Hill Mafinga tarehe 19 Machi 2012

Ndugu Wadau wa Misitu,

Natumia fursa hii kuwafahamisha kuwa kuongezeka kwa mahitaji ya mazao ya misitu, kumesababisha msukumo mkubwa kwa wananchi kutaka kuvuna mazao ya misitu kutoka kwenye mashamba ya misitu ya serikali. Kutokana na msukumo huo wa mahitaji ni dhahiri kuwa mabadiliko ya haraka yanahitajika ili kusimamia ipasavyo uzalishaji, uvunaji na usimamizi wa bei ya mazao ya misitu. Mabadiliko haya yatafanikishwa na wadau wa mazo ya misitu, hususan Sekta Binafsi na Wakala wa Misitu Tanzania (Tanzania Forest Service – TFS).

Katika miaka mitatu iliyopita, uzalishaji wa mbao umeshuka kutoka mita za ujazo 1,500,000 hadi 1,200,000. Kufuatia kukua kwa uchumi watu wengi sasa wanahitaji kujenga nyumba za kisasa, hivyo mahitaji halisi ya mbao kwenye soko yameongezeka kutoka mita za ujazo 2,000,000 hadi 5,000,000. Ongezeko hili limetokana pia na  kupanuka kwa soko la nje hasa katika nchi za Kenya, Djibouti, Sudan Kusini, Uarabuni na India.

Pamoja na ongezeko hili la soko na kushuka kwa uzalishaji, hadi sasa  hakuna mabadiliko katika jitihada za kuongezeka kwa uzalishaji, wala Serikali haijanufaika na ongezeko hilo la soko kwa sababu bei imeshuka kwa asilimia thelathini (30%) kutoka bei ya juu ya mwaka 2007. Hali hii imesababisha utitiri wa waombaji wa mazao ya misitu na malalamiko mengi kuhusu ugawaji wa vibali vya uvunaji.

Kwa hiyo Serikali imeamua kufanya mabadiliko ya muda mfupi ya utaratibu wa utoaji vibali kwa kuanzisha fomu maalum ambayo itajazwa na  waombaji. Hata hivyo, mabadiliko haya ni ya muda tu. Bado mabadiliko makubwa ya muda mrefu yanahitajika.
Maeneo yanayohitajika kufanyiwa mabadiliko ni kama ifuatavyo::-

1. Kuongeza mapato ya Serikali kwa kurekebisha bei ya tozo za Serikali angalau zifikie gharama halisi za uzalishaji. Kwa sasa, bei ya kuuzia ni 54% ya gharama halisi ya uzalishaji wa miti ya kutengenezea karatazi (“pulp”) na asilimia 90 kwa miti ya mbao.

2. Kuongeza mapato ya Serikali kwa kurekebisha bei ya vibali vya kusafirishia nje ya nchi (export permits). Hii ni kwa lengo la kuifanya nchi ifaidike na soko kubwa la nje na kukatisha tamaa ya kuuza mbao nje ya nchi, hivyo kupunguza bei za mbao hapa nchini.

Aidha, Wakala wa Hudma za Misitu Tanzania (TFS) umetakiwa kuimarisha ukaguzi katika mipaka kwa kuanzisha vituo na kupeleka watumishi katika vituo vyote vya mipakani. Kwa sasa kazi hiyo ya ukaguzi inafanywa na Maafisa Kodi wa TRA.

3. Kuweka udhibiti wa bei kwa kuanzisha mfumo wa uzalishaji na usambazaji wa jumla na rejareja kwa kuanzisha mawakala watakaopatikana kwa tenda ambao watauza mazao ya misitu kwa bei elekezi itakayowekwa na Serikali.

4. Kuongeza uzalishaji kwa kuweka mikataba na mawakala ya kuwataka wawe na mashamba yao katika kipindi cha miaka 15 - 20. Kwa kufanya hivyo baada ya miaka 20 ijayo, angalau asilimia arobaini (40%) ya malighafi za mbao itakuwa inatoka kwenye mashamba binafsi. Kwa sasa asilimia tisini na nane (98%) ya mbao zinatoka kwenye mashamba ya miti na hifadhi za misitu ya serikali.

Ili kufikia hatua hii, mikataba iliyopo kati ya Serikali na wawekezaji itabidi irekebishwe au ivunjwe. Majadiliano kuhusu suala hili, yanatakiwa yaanze sasa na mikataba mipya iwekwe kati ya sasa na mwaka 2014.

5. Mapungufu ya kimkataba na kiusimamizi yanayofanya wawekezaji wakubwa kuuziwa malighafi kwa bei ya chini, huku wavunaji wadogo wakiuziwa malighafi hizo hizo kwa bei ya juu yatarekebishwa kuanzia msimu ujao, Julai 2012. Aidha, ili kufikia lengo la kuzalisha karatasi kamili hapa nchini, ruhusa ya kusafirisha karatasi ambazo hazijafikia kiwango cha mwisho cha etengenezaji (“semi-processed papers”)  itaangaliwa upya.

6. Ili kuimarisha matumizi ya malighafi kidogo zilizopo, Wakala wa Misitu Tanzania - TFS unatakiwa kuanza utaratibu wa kugawa malighafi kwa kutazama matumizi ambapo wavunaji watakuwa wanapewa malighafi kwa kipindi kifupi, yaani kwa mwezi. Baada ya kuvuna na  na kumaliza kutumia, mvunaji ataandaa taarifa itakayoonyesha malighafi hiyo ilivyotumika ndipo aweze kupewa  mgao mwingine unaofuata.

Mabadiliko hayo ni badala ya kupewa mgao wa mwaka mzima ambao wahusika huwa hawana uwezo wa kuutumia wote, badala yake wanawauzia watu wengine kwa ulanguzi. Aidha, TFS ianzishe utaratibu wa kugawa malighafi za “chips” kwa kiwanda cha karatasi cha Mufindi Paper Mill (MPM), badala ya kugawa malighafi ya miti iliyokomaa kama inavyofanyika hivi sasa.

7. Ili kuongeza motisha na uzalishaji kwa wananchi waishio jirani na mashamba ya miti, TFS ianzishe utaratibu wa kuwasaidia walimaji wadogo wa miti. Kadiri itakavyowezekana, misaada ya ujirani mwema itakayotolewa na TFS kwa wananchi ilenge katika kuimarisha sekta ya misitu.

Aidha, Mfuko wa Misitu Tanzania (Tanzania Forest Fund -  TFF) uimarishwe kwa kuongezewa vyanzo vya mapato kwa kushirikisha wadau wa maendeleo. Pia mfuko huo uimarishwe kiutendaji kwa kuwa na menejimenti yake ambayo itakuwa inatoa  mikopo ya muda mrefu na ruzuku kwa wakulima wadogo wa miti.

8. Ili kuongeza ulinzi kwenye mashamba ya Serikali, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) uweke mkakati maalum wa kubainisha mipaka na kuilinda. Pia, TFS iandae mkakati maalum wa kupanda miti kwa maeneo yasiyo na miti, ama, kwa kupanda wenyewe au kutumia sekta binafsi kwa mikataba maalum ya muda mrefu (long term concessations).

Kwa mfano, Shamba la Miti la Sao Hill linaweza kuingia mikataba ya muda mrefu na wadau maana ukubwa wa shamba hilo ni hekta 130,000, lakini zilizopandwa miti hadi sasa ni takriban hekta 50,000 tu.

Yapo maeneo mengi yanayoweza kuwekewa mikataba ya kupanda miti, kama vile mashamba ya Serikali ya Buhindi mkoani Mwanza na Rubare mkoani Kagera.

9. Ili kukabiliana na changamoto ya uvamizi wa maeneo ya hifadhi na mashamba ya miti, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) uanzishe dawati maalum la kusimamia migogoro kwa majadiliano na kwa kutumia taratibu za kisheria.

Imetolewa na Mhe. Ezekiel M. Maige (Mb)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII.
19 Machi 2012

No comments:

Post a Comment